Mohamed Faik: Kutoka Mwanaharakati wa Haki za Binadamu hadi Mwanadiplomasia Maarufu katika Uwanja wa Kimataifa
Imetafsiriwa na: Diaa El-Din Mohamed
Imehaririwa na: Mervat Sakr
Mratibu wa Lugha ya Kiswahili: Mervat Sakr
Tangu alipoanza safari yake ya kikazi, Mohamed Faik ameonyesha kuwa ni moja ya nyota muhimu zaidi katika uwanja wa diplomasia na haki za binadamu katika ulimwengu wa Kiarabu. Sio tu kwa sababu alishikilia nyadhifa muhimu nchini Misri na katika ulimwengu wa Kiarabu, bali pia kwa sababu daima alikuwa mstari wa mbele katika kutetea haki za binadamu, akiwa na mchango mkubwa katika masuala muhimu yanayogusa jamii za Kiarabu na Kiafrika.
Mohamed Faik amewahi kushikilia nyadhifa nyingi muhimu, na alikuwa na ushawishi mkubwa kuhusu haki za binadamu katika ulimwengu wa Kiarabu. Hivi sasa anashikilia nafasi ya Mwenyekiti wa Baraza la Kitaifa la Haki za Binadamu nchini Misri, ambapo anahusika na kusimamia na kufuatilia hali ya haki za binadamu nchini humo. Pia ni Makamu wa Rais wa Kamati ya Kidemokrasia ya Misri kwa mshikamano wa Afrika na Asia, na anachukuliwa kama mmoja wa wanachama mashuhuri katika kukuza ushirikiano kati ya watu wa Afrika na Asia.
Miongoni mwa nyadhifa muhimu alizowahi kushikilia hapo awali ni pamoja na kuwa mwanachama wa Kamati ya Uchunguzi ya Umoja wa Mataifa kuhusu Darfur, ambapo alifuatilia hali ya kibinadamu katika eneo hilo lenye machafuko. Aidha, aliwahi kuwa Kamishna wa Haki za Binadamu katika Umoja wa Afrika, wadhifa uliompa nafasi ya kuchangia kikamilifu katika bara la Afrika kupitia utoaji wa suluhu na mipango ya kuimarisha haki za binadamu.
Mohamed Faik si mtetezi wa haki za binadamu pekee, bali pia ni mwanadiplomasia hodari na kiongozi mashuhuri katika uwanja wa kisiasa wa kimataifa. Amewahi kushiriki kama mwakilishi wa Misri katika mikutano kadhaa ya kimataifa, ikiwa ni pamoja na mikutano ya kilele ya Afrika kwa miaka kadhaa, na pia alikuwa sehemu ya diplomasia ya Misri katika Umoja wa Mataifa, ambapo aliwakilisha nchi yake katika Kamati ya Nne ya Mkutano Mkuu.
Faik pia alikuwa na mchango mkubwa katika kusaidia harakati za ukombozi barani Afrika, daima akiwa mhamasishaji thabiti wa uhuru wa kisiasa na kiuchumi wa bara hilo. Kuanzia mwaka 1953 hadi miaka ya sabini, Faik alishirikiana kwa karibu na harakati za ukombozi barani Afrika, akiwa sehemu ya vuguvugu lililotafuta kukomesha ukoloni katika mataifa mengi ya Kiafrika.
Mbali na majukumu yake ya kisiasa na kidiplomasia, Mohamed Faik pia alikuwa na mchango muhimu katika nyanja za utafiti na taaluma. Miongoni mwa kazi zake muhimu ni kitabu chake mashuhuri “Abdel Nasser na Mapinduzi ya Kiafrika”, ambacho kilijadili uhusiano wa kiongozi wa Misri, Gamal Abdel Nasser, na harakati za ukombozi barani Afrika pamoja na mchango wake katika kuimarisha mapinduzi ya Kiafrika dhidi ya ukoloni.
Pamoja na nyadhifa na mafanikio haya yote, Faik anaendelea kuwa mfano wa kuigwa katika kudumisha usawa kati ya siasa na haki za binadamu. Pia aliwahi kuwa Katibu Mkuu wa Shirika la Kiarabu la Haki za Binadamu, na Mwenyekiti wa Bodi ya Gazeti la Al-Arabi, pamoja na kushikilia nyadhifa nyingi za uwaziri katika maisha yake, ikiwemo Waziri wa Habari na Waziri wa Nchi kwa Mambo ya Nje.
Hivi karibuni, Faik bado anaendelea kuwa na mchango mkubwa katika masuala ya haki za binadamu, iwe ni katika uwanja wa kitaifa au wa kikanda. Ushawishi wake haukuishia Misri pekee, bali ulipanuka kuufikia ulimwengu wa Kiarabu na bara la Afrika.
Mwishowe, Mohamed Faik anabaki kuwa mmoja wa nguzo za diplomasia ya Kimasri na Kiarabu, na alama ya kujitolea kwa dhati katika masuala ya haki za binadamu kwa miongo kadhaa.